TAMBWE APEWA TANO NA STAA HUYU KUTOKA SIMBA

 Former Simba SC forward Emmanuel Okwi

Wakati kikosi cha Simba kikikaribia kutangaza ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu, mshambuliaji wa timu hiyo, Mganda, Emmanuel Okwi ametoa kauli ya kummwagia sifa mshambuliaji wa Yanga, Mrundi, Amissi Tambwe.

Okwi ambaye anaongoza msimu huu katika michuano ya Ligi Kuu Bara kwa kuzifumania nyavu akiwa na mabao 20, amemmwagia sifa Tambwe kutokana na kazi kubwa aliyoifanyia Yanga msimu wa 2015/16.

Katika msimu huo, Tambwe alifanikiwa kuifungia timu yake hiyo ya Yanga mabao 21, huku pia akifanikiwa kuwa mfungaji bora.

Kwa mujibu wa gazeti la Championi Jumatano, Okwi alisema kuwa amefikia hatua hiyo ya kumpongeza Tambwe kutokana na kuitambua kazi kubwa aliyoifanyia Yanga msimu huo lakini pia heshima ambayo alitoa hivi karibuni dhidi yake baada ya kufanikiwa kuzivunja baadhi ya rekodi zake za kuzifumania nyavu pamoja na za wachezaji wengine.

“Siku zote unapofanikiwa kufunga unakuwa umeisaidia timu yako kufanya vizuri, lakini pia unapofanikiwa kuvunja rekodi za waliokutangulia ni jambo zuri.

“Namshukuru sana Tambwe kwa heshima ambayo amenipatia baada ya kuvunja baadhi ya rekodi zake, lakini pia na mimi napongeza sana kwa kazi kubwa aliyoifanyia Yanga msimu wa 2015/16.

“Kuhusiana na kuivunja rekodi yake hiyo ya mabao 21 hakika anayejua hilo ni Mungu kwani lolote linaweza kutokea katika mechi hizi zilizobakia ila jambo kubwa ambalo naweza kusema ni kwamba nitaendelea kupambana kwa kushirikiana na wachezaji wenzangu ili kuhakikisha tunapata matokeo mazuri katika mechi zetu zilizobakia.

“Ikitokea nikaivunja rekodi hiyo basi nitamshukuru Mungu pia,” alisema Okwi.

CHANZO KUTOKA; SALEHE JEMBE